Ijumaa, 22 Novemba 2013

DHAMBI

Dhambi ni uasi, 1Yoh 3:4; Isa 1:2; Zab 51:4; Kum 9:18.
Dhambi inaweza kutokea kwa namna mbalimbali kuanzia kwa matendo maovu, kwa makusudi mpaka kwa bahati mbaya, kwa sababu ya udhaifu, uvivu au kutokujua, Kut 32:30; Mt 5:22,28; Mit 28:13; Rum 1:29-32, 3:23; Yak 4:17.

ASILI YA DHAMBI
Kutokana na shughuli za shetani katika bustani ya Edeni inaonekana wazi kuwa dhambi ilikuwapo ulimwenguni kabla ya Adamu na Hawa hawajatenda dhambi, lakini Biblia haielezi jinsi dhambi ilivyoanza kwa asili yake bali inaeleza tu jinsi ilivyoingia kwa mwanadamu. Mwanadamu alivuka mpaka ambao Mungu alimwekea, hivyo alianguka katika dhambi. Kiburi kilikuwa kiini cha dhambi ya mwanadamu, 1Yoh 2:16; Rum 1:21-23.
Dhambi ilingia kwa sababu mwanadamu alianza kumtilia mashaka Mungu, Yak 1:14. Dhambi ilianzia moyoni mwake na tendo la kutokuamini lilikuwa matokeo yake ya lazima, Yer 17:9; Mwa 6:5.

MATOKEO YA DHAMBI
Mwanadamu alianguka chini ya hukumu ya Mungu na kuingia hali ya uadui dhidi ya:-
            1. Ulimwengu wa viumbe, Mwa 3:17-19.
            2. Wanadamu wenzake, Mwa 3:12,13; 1Yoh 3:12.
            3. Nafsi yake mwenyewe, Mwa 3:7, 11-13; Rum 7:15,19.
            4. Mungu, Mwa 3:8-10, 22-24; Rum 3:10-18.
Adhabu kuu ya dhambi ni mauti, Mwa 2:17; 3:19,24; Rum 6:23. Mauti haikuwa ya kimwili tu bali pia ya kiroho, ambayo ni kutengwa na Mungu ambaye ni asili ya chemchemi ya uzima wa kiroho, Rum 6:16,17, 5:13; 1Kor 15:56.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni