Jumanne, 9 Desemba 2014

ADUI

Adui ni mtu mtu yeyote au roho yoyote iliyo kinyume na wewe yenye lengo au nia ya kuzuia maendeleo yako kimwili na kiroho.
TABIA ZA ADUI
i. Muongo, Yn 8:44c.
ii. Mjaribu, Mt 4:3; 1Thes 3:5.
iii. Mwivi, Yn 10:10.
iv. Muuaji, Yn 8:44b
v. Mpotoshaji, Mwa 3:4, 5.
vi. Mgawanyaji, Mt 26:31; Zek 13:7.
vii. Kama malaika wa nuru, 2Kor 11:14, 15.
Kila mkristo anao maadui wakuu watatu ambao ni:-
1. DUNIA
Biblia imetumia neno dunia katika nyanja tatu tofauti.
Mosi, limetumika kuzungumzia dunia ambayo Mungu kaiumba, Mdo 17:24.
Pili, linazungumzia watu, Yn 3:16.
Tatu, matumizi ya neno hili yanapatikana katika 1Yoh 2:15. Neno dunia hapa limetumika kuelezea “mfumo wa dunia”, adui wa kila mwana wa Mungu. Hii ndiyo fasili ya dhana ambayo tutakuwa tunatumia neno “dunia” katika somo hili.
Shetani amepanga watu na vitu kwenye mfumo wa dunia chini ya ubinafsi, kiburi, uloho/ulafi na tamaa za dhambi. Mfumo wa dunia wa shetani unajumuisha burudani, biashara, elimu, dini, siasa, falme za dunia, mashirika ya kiulimwengu na vyombo vya habari. Shetani anawadanganya watu katika kufikiri kwamba dunia hii ndiyo jambo la pekee linalofaa. Katika huu mfumo wa dunia shetani anaweza kuwapa watu utajiri, milki, nguvu, umaarufu na tamaa zote za dhambi. Shetani anawaruhusu watu kufanya mambo na kutoa maamuzi, lakini yeye mwenyewe ni kiongozi asiyeonekana wa dunia hii, 1Yoh 5:19. Shetani anajua kuwa hawezi akawazuia wakristo kuenda mbinguni lakini kusudi lake ni kuwafanya wafuate mambo ya dunia. Anawataka wafikiri kama watu wa dunia na watende mambo yale yale yafanywayo na watu wa dunia hii.
Maandiko katika 1Yoh 2:16, 17, yameyagawanya mambo ya dunia hii katika makundi matatu ambayo ni:-
i. Tamaa ya mwili (utamanifu, upenda anasa)
Ni tamaa (kutamani) ya kitu chochote kinachopendeza/furahisha/anisi akili. Tunaporuhusu tamaa za mwili kutenda kazi isivyo halali – mambo haya ni dhambi na ni ya kidunia.
ii. Tamaa ya macho (uyakinifu, tamaa ya vitu)
Ni tamaa/shauku ya kumiliki vile tuvionavyo. Ni tamaa binafsi inayotokea wakati tunapoviona vitu ambavyo ni dhahiri kuwa hatuvihitaji ila tunavitaka, ni hamu ya kumiliki, shauku ya kupata.
iii. Kiburi cha uzima (majisifu, ubinafsi)
Ni tamaa ya kuongeza faida ya mtu na kujiinua, tamaa ya kuhamakisha sifa zake, jaribio la kufanya waa ling’are ndani yetu. Kiburi cha uzima ni kitendo cha kujiweka juu kuwa wewe ni mtu fulani.
2. MWILI
Ni hali yetu ya ubinadamu iliyo na hali ya asili ya dhambi. Neno “Mwili” wakati mwingine katika Biblia limetumika kuelezea “nyama.” Lakini hapa neno “mwili” linazungumzia (utu wetu wa kale) hali yetu ya anguko.
Biblia inatueleza kuwa tumezaliwa tukiwa na mioyo ya dhambi na inatufanya tutende dhambi katika maisha yetu yote. Mkristo ana asili mbili – maisha mapya (utu mpya) aliyoyapokea wakati alipomkubali Kristo Yesu, na utu wa kale uitwao “mwili.” Utu mpya huongozwa na Roho Mtakatifu, utu wa kale umebainishwa na tamaa za dhambi. Wakati utu mpya unapowekwa sambamba na utu wa kale uliokengeuka ambao tulizaliwa nao kuna vita, Gal 5:17. Mwili hushindana na mamlaka, huchoka, ni rahisi kuendeleza mawazo ya kisasi, umeelekea kwenye kuabudu (nguvu zetu, ujanja wetu, mawazo yetu na mwonekano wetu). Haya yote ni matamanio ya mwili yanayohitaji kuongozwa kwa msaada wa Roho wa Mungu.
3. SHETANI
Shetani ni amiri jeshi mkuu wa mapepo anayempinga Mungu, na amejitoa kufanya kazi ya kuwaangamiza wale walioukubali wokovu wa Bwana Yesu. Biblia inamweleza kuwa ni mdanganyifu, mwongo, muuaji, mshitaki, mjaribu, mwovu. Hulaghai, hupotoa, hupinga, hudanganya, hupanda magugu, huzuia, hujaribu na kukufuru. Ni mjanja, ni mharibifu, ana injili yake, Gal 1:6; ana kanisa lake, Ufu 2:9; ana watumishi wake, 2Kor 11:15; ana mafundisho yake, 1Tim 4:1; ana ushirika wake, 1Kor 10:21. Shetani anaweza fanya yote, anaweza kuzuia maisha yetu ya Kikristo. Shambulio la shetani haliwezi kuja kwa njia ya wazi na rahisi kuonekana, huwa erevu, pambanuzi. Shetani hutumia vivutio vya dunia na tamaa za mwili kutujaribu na kutupata ili tutende dhambi.
NJIA AMBAZO ADUI HUZITUMIA KUWAANGUSHA WAKRISTO
1. Uchovu
Esau ni mfano amilifu wa mtu ambaye hakuchukua tahadhari kwa sababu alikuwa amechoka. Baada ya kuwinda porini alirudi nyumbani akiwa amechoka, akamkuta Yakobo akiandaa chakula, harufu nzuri ya makande yaliamsha maonjo kinywani mwake, alikuwa tayari kufanya chochote ili mradi tu ale. Aligundua kuwa mdogo wake angempa chakula kama angemuuzia haki yake ya uzaliwa wa kwanza. Kitambo kidogo tu katika udhaifu wa mwili, Esau akauza urithi wake kwa kande la dengu, Mwa 25:29-34.
2. Furaha
Jaribu laweza kuja katikati ya furaha yetu. Mfalme Herode ni mfano madhubuti wa mtu aliyekamatwa katika mtego wake. Wakati wa usiku wa sherehe yake ya kuzaliwa katika kasri lake, aliathiriwa kwa urahisi kutokana na tamaa ya binti aliyekuwa anacheza, alikuwa akifurahia pombe, tamaa ya kitambo tu, walakini katika saa iyo hiyo ya furaha ya hatari, akatoa sadaka badhirifu, Mt 6:23.
3. Mashaka
Mfano mzuri ni Petro alipojaribu kutembea juu ya maji baharini na akina mama waliokuwa wakielekea kaburini kuupaka marhamu mwili wa Yesu, Shetani aliwafanya waliangalie tatizo, Mt 14:29, 30; Mk 16:2.
4. Kazi nyingi, Lk 8:14; 1Yoh 5:2.
5. Mashutumu, Mwa 3:12, 13.
6. Matumizi mabaya ya ulimi, Yak 3:2, 5, 6.
7. Kukosa msimamo katika imani, Kumb 29:18; Ebr 12:15.
8. Kusinzia katika ibada, semina, mikutano au maombi, Mdo 20:9.
JINSI YA KUMPINGA
1. Uongozwe na Neno
Lifanye Neno la Mungu kuwa kiongozi wako na ukubali likutawale na uishi kwa kila kitu lisemacho. Litakuwezesha kuenenda kwa unyoofu wa moyo na kukulinda na aina zote za majaribu, Zab 119:9, 105.
2. Kumvaa Kristo, Rum 13:14.
3. Kutembea katika roho, Gal 5:16.
4. Kujihesabu kuwa mfu kwa dhambi, Rum 6:11.
5. Tumia jina la Yesu, Flp 2:10, 11; Kol 1:13.
6. Kuomba, Efe 6:18.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni