Jumanne, 9 Desemba 2014

ADUI

Adui ni mtu mtu yeyote au roho yoyote iliyo kinyume na wewe yenye lengo au nia ya kuzuia maendeleo yako kimwili na kiroho.
TABIA ZA ADUI
i. Muongo, Yn 8:44c.
ii. Mjaribu, Mt 4:3; 1Thes 3:5.
iii. Mwivi, Yn 10:10.
iv. Muuaji, Yn 8:44b
v. Mpotoshaji, Mwa 3:4, 5.
vi. Mgawanyaji, Mt 26:31; Zek 13:7.
vii. Kama malaika wa nuru, 2Kor 11:14, 15.
Kila mkristo anao maadui wakuu watatu ambao ni:-
1. DUNIA
Biblia imetumia neno dunia katika nyanja tatu tofauti.
Mosi, limetumika kuzungumzia dunia ambayo Mungu kaiumba, Mdo 17:24.
Pili, linazungumzia watu, Yn 3:16.
Tatu, matumizi ya neno hili yanapatikana katika 1Yoh 2:15. Neno dunia hapa limetumika kuelezea “mfumo wa dunia”, adui wa kila mwana wa Mungu. Hii ndiyo fasili ya dhana ambayo tutakuwa tunatumia neno “dunia” katika somo hili.
Shetani amepanga watu na vitu kwenye mfumo wa dunia chini ya ubinafsi, kiburi, uloho/ulafi na tamaa za dhambi. Mfumo wa dunia wa shetani unajumuisha burudani, biashara, elimu, dini, siasa, falme za dunia, mashirika ya kiulimwengu na vyombo vya habari. Shetani anawadanganya watu katika kufikiri kwamba dunia hii ndiyo jambo la pekee linalofaa. Katika huu mfumo wa dunia shetani anaweza kuwapa watu utajiri, milki, nguvu, umaarufu na tamaa zote za dhambi. Shetani anawaruhusu watu kufanya mambo na kutoa maamuzi, lakini yeye mwenyewe ni kiongozi asiyeonekana wa dunia hii, 1Yoh 5:19. Shetani anajua kuwa hawezi akawazuia wakristo kuenda mbinguni lakini kusudi lake ni kuwafanya wafuate mambo ya dunia. Anawataka wafikiri kama watu wa dunia na watende mambo yale yale yafanywayo na watu wa dunia hii.
Maandiko katika 1Yoh 2:16, 17, yameyagawanya mambo ya dunia hii katika makundi matatu ambayo ni:-
i. Tamaa ya mwili (utamanifu, upenda anasa)
Ni tamaa (kutamani) ya kitu chochote kinachopendeza/furahisha/anisi akili. Tunaporuhusu tamaa za mwili kutenda kazi isivyo halali – mambo haya ni dhambi na ni ya kidunia.
ii. Tamaa ya macho (uyakinifu, tamaa ya vitu)
Ni tamaa/shauku ya kumiliki vile tuvionavyo. Ni tamaa binafsi inayotokea wakati tunapoviona vitu ambavyo ni dhahiri kuwa hatuvihitaji ila tunavitaka, ni hamu ya kumiliki, shauku ya kupata.
iii. Kiburi cha uzima (majisifu, ubinafsi)
Ni tamaa ya kuongeza faida ya mtu na kujiinua, tamaa ya kuhamakisha sifa zake, jaribio la kufanya waa ling’are ndani yetu. Kiburi cha uzima ni kitendo cha kujiweka juu kuwa wewe ni mtu fulani.
2. MWILI
Ni hali yetu ya ubinadamu iliyo na hali ya asili ya dhambi. Neno “Mwili” wakati mwingine katika Biblia limetumika kuelezea “nyama.” Lakini hapa neno “mwili” linazungumzia (utu wetu wa kale) hali yetu ya anguko.
Biblia inatueleza kuwa tumezaliwa tukiwa na mioyo ya dhambi na inatufanya tutende dhambi katika maisha yetu yote. Mkristo ana asili mbili – maisha mapya (utu mpya) aliyoyapokea wakati alipomkubali Kristo Yesu, na utu wa kale uitwao “mwili.” Utu mpya huongozwa na Roho Mtakatifu, utu wa kale umebainishwa na tamaa za dhambi. Wakati utu mpya unapowekwa sambamba na utu wa kale uliokengeuka ambao tulizaliwa nao kuna vita, Gal 5:17. Mwili hushindana na mamlaka, huchoka, ni rahisi kuendeleza mawazo ya kisasi, umeelekea kwenye kuabudu (nguvu zetu, ujanja wetu, mawazo yetu na mwonekano wetu). Haya yote ni matamanio ya mwili yanayohitaji kuongozwa kwa msaada wa Roho wa Mungu.
3. SHETANI
Shetani ni amiri jeshi mkuu wa mapepo anayempinga Mungu, na amejitoa kufanya kazi ya kuwaangamiza wale walioukubali wokovu wa Bwana Yesu. Biblia inamweleza kuwa ni mdanganyifu, mwongo, muuaji, mshitaki, mjaribu, mwovu. Hulaghai, hupotoa, hupinga, hudanganya, hupanda magugu, huzuia, hujaribu na kukufuru. Ni mjanja, ni mharibifu, ana injili yake, Gal 1:6; ana kanisa lake, Ufu 2:9; ana watumishi wake, 2Kor 11:15; ana mafundisho yake, 1Tim 4:1; ana ushirika wake, 1Kor 10:21. Shetani anaweza fanya yote, anaweza kuzuia maisha yetu ya Kikristo. Shambulio la shetani haliwezi kuja kwa njia ya wazi na rahisi kuonekana, huwa erevu, pambanuzi. Shetani hutumia vivutio vya dunia na tamaa za mwili kutujaribu na kutupata ili tutende dhambi.
NJIA AMBAZO ADUI HUZITUMIA KUWAANGUSHA WAKRISTO
1. Uchovu
Esau ni mfano amilifu wa mtu ambaye hakuchukua tahadhari kwa sababu alikuwa amechoka. Baada ya kuwinda porini alirudi nyumbani akiwa amechoka, akamkuta Yakobo akiandaa chakula, harufu nzuri ya makande yaliamsha maonjo kinywani mwake, alikuwa tayari kufanya chochote ili mradi tu ale. Aligundua kuwa mdogo wake angempa chakula kama angemuuzia haki yake ya uzaliwa wa kwanza. Kitambo kidogo tu katika udhaifu wa mwili, Esau akauza urithi wake kwa kande la dengu, Mwa 25:29-34.
2. Furaha
Jaribu laweza kuja katikati ya furaha yetu. Mfalme Herode ni mfano madhubuti wa mtu aliyekamatwa katika mtego wake. Wakati wa usiku wa sherehe yake ya kuzaliwa katika kasri lake, aliathiriwa kwa urahisi kutokana na tamaa ya binti aliyekuwa anacheza, alikuwa akifurahia pombe, tamaa ya kitambo tu, walakini katika saa iyo hiyo ya furaha ya hatari, akatoa sadaka badhirifu, Mt 6:23.
3. Mashaka
Mfano mzuri ni Petro alipojaribu kutembea juu ya maji baharini na akina mama waliokuwa wakielekea kaburini kuupaka marhamu mwili wa Yesu, Shetani aliwafanya waliangalie tatizo, Mt 14:29, 30; Mk 16:2.
4. Kazi nyingi, Lk 8:14; 1Yoh 5:2.
5. Mashutumu, Mwa 3:12, 13.
6. Matumizi mabaya ya ulimi, Yak 3:2, 5, 6.
7. Kukosa msimamo katika imani, Kumb 29:18; Ebr 12:15.
8. Kusinzia katika ibada, semina, mikutano au maombi, Mdo 20:9.
JINSI YA KUMPINGA
1. Uongozwe na Neno
Lifanye Neno la Mungu kuwa kiongozi wako na ukubali likutawale na uishi kwa kila kitu lisemacho. Litakuwezesha kuenenda kwa unyoofu wa moyo na kukulinda na aina zote za majaribu, Zab 119:9, 105.
2. Kumvaa Kristo, Rum 13:14.
3. Kutembea katika roho, Gal 5:16.
4. Kujihesabu kuwa mfu kwa dhambi, Rum 6:11.
5. Tumia jina la Yesu, Flp 2:10, 11; Kol 1:13.
6. Kuomba, Efe 6:18.

Jumamosi, 3 Mei 2014

KUTEMBEA KATIKA ROHO




Gal 5:25
i.        Kutembea katika Roho ni kutekeleza maamuzi ya Roho na kuishi ndani ya mwongozo wake na si kuenenda au kuingiza au kujaribu kurekebisha au kubadilisha mwongozo.
ii.      Kutembea katika Roho ni kufanya mambo yale ambayo torati na mwili vimeshindwa kuyafanya.

MAMBO YA KUZINGATIA KATIKA KUTEMBEA KATIKA ROHO
1.    UJUE UDHAIFU WAKO, Yak 3:2
Jambo hili ni la muhimu sana na kamwe halipaswi kupuuzwa. Unatakiwa kuubaini udhaifu wako kwa sababu kweli iliyomo ndani yako ni adui na inaujua udhaifu wako kuliko wewe. Lielewe eneo hili kwa makini na umkabidhi Roho Mtakatifu ambaye ni rafiki mwema na mnasihi wa milele naye atakutia nguvu na kukusaidia kuutambua na kuzuia majaribu na vishawishi.
2.    YAFISHE MATENDO YA MWILI KWA ROHO, Rum 8:3
Mtu ambaye amefanywa upya na Roho hawezi kunaswa katika dhambi. Kwa Roho, tamaa za mwili zinashindwa. Kuyafisha matendo ya mwili ni adhimu ni sawa na kusema “dhambi hapana” lakini ni tofauti na kampeni ya kupambana na madawa ya kulevya miongoni mwa vijana miaka mingi iliyopita. Kusema “dhambi hapana” pekee haitafanikiwa, kusema “dhambi hapana kamwe huwezi ukashinda dhambi. Je nini unatakiwa ufanye? Sema “hapana Kwa Roho.
3.    UONGOZWE NA ROHO, Rum 8:14; Efe 5:15
Roho mtakatifu hutuongoza wakati wote. Hutuongoza kupitia neno lake lililofunuliwa kwa manabii, 2Pet 1:20, 21. Tunapaswa kuwa waangalifu, waombaji na wanyenyekevu katika kutumia hekima pana ya Biblia katika hali tunazokutana nazo. Wakati mwingine Roho Mtakatifu hutuongoza moja kwa moja. Roho Mtakatifu anaweza kutenda kwa njia yoyote, kulingana ratiba yoyote kama apendavyo. Hatumwongozi namna au wakati gani atembee. Biblia imebainisha mifano mingi ya jinsi Roho Mtakatifu anavyoweza kutenda, tunapaswa kukubali kuwa wakati mwingine aweza kuchagua kutuongoza moja kwa moja kama tutakuwa huru na tu katika mwongozo wake.
4.    UJUE U BABA WA MUNGU  KWA ROHO Rum 8:15-17
Pasipo Roho Mtakatifu tusingeujua utambulisho wetu kuwa tu wana wa Mungu. Ashukuriwe Mungu aliyetupatia Roho Mtakatifu bure, na mistari hii kutoka Rum 8 inaonesha mambo matatu ya ajabu ambayo Roho Mtakatifu ameyafanya:
a.    Anatenda kama kiunganishi ambaye ametutoa mahali pa utumwa na hofu na kutuleta mahali pa kupitishwa na kukubaliwa.
b.    Anatusaidia kulia “ABBA” yaani baba.
c.    Anashuhudia na roho zetu kuwa tu wana wa Mungu.
5.    OMBA KATIKA ROHO, Rum 8:26-28
Mistari hii miwili (Rum 8:26,27)  ina utajiri mwingi na inatusaidia katika kuishi kwetu katika Roho.
a.    Tunajifunza kuwa tu dhaifu tunapokuwa katika kuomba. Hatujui kuomba katika hali yoyote.
b.    Tunajifunza kuwa Roho huungana kutusaidia tunapotaka kujua jinsi ya kuomba kwa ktuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa.
c.    Roho huchunguza mioyo yetu na kujua akili zetu kwamba zimeelekezwa kwake hata kama hatujui namna ya kuomba.
d.    Matokeo ni kwamba maombi yetu yanaomba “kulingana na mapenzi na Mungu”  kwa sababu Roho Mtakatifu (anatembea katikati yetu) anatuongoza kuomba na kuyawasilisha maombi yetu kwa baba.
FAIDA ZA KUTEMBEA KATIKA ROHO
1.    Kuwekwa huru mbali na sheria ya dhambi na mauti, Rum 8:2-4.
2.    Kuwa hekalu la Roho Mtakatifu, 1Kor 6:19.
3.    Kuyajua mafumbo ya Mungu, 1Kor 2:10-15.
4.    Kushirikishwa uzima wa milele, Yn 3:5; Efe 2:5.
5.    Kuongozwa na roho, Lk 2:25, 26; Mdo 13:4, 16:6-10.
6.    Kuthibitishwa kuwa wana wa Mungu, Rum 8:16.
7.    Roho Mtakatifu kusema nasi, Mdo 10:19.
8.    Kuwa mashahidi, Mdo 5:32; Yn: 16, 17.

Ijumaa, 21 Machi 2014

ROHO MTAKATIFU


Roho mtakatifu ni nafsi ya tatu katika uungu.

   A: JINSI TUHAKIKISHAVYO KUWA ROHO MTAKATIFU NI NAFSI MOJA
1.      Roho Mtakatifu anadhihirishwa kuwa na akili na hekima
-  Anaelimisha watu wa Mungu, Neh 9:20.
-  Anafundisha wakristo, Lk 12:11, 12.
-  Anakumbusha yote, Yn 14:26.
-  Anatoa karama za hekima na maarifa, 1Kor 12:8.
2.      Roho Mtakatifu anajionea mambo mbalimbali peke yake
-  Nia yake haipatani na nia ya mwili, Rum 8:6.
-  Anaweza kuhuzunika na kuhuzunishwa, Isa 63:10.
-  Anatutamani kwa utakatifu kiasi cha kuona wivu, Yak 4:5, 6.
-  Akikufuriwa hakuna msamaha, Mt 12:30, 31.
3.      Roho Mtakatifu anakuwa na mapenzi na kusudi lake
-  Akigawa karama zake , anatenda kama apendavyo, 1Kor 12:11.
4.      Roho Mtakatifu anasema na watu
-  Alimwambia Filipo kusogea karibu na gari la Mkushi, Mdo 8:29.
-  Alimwambia mtume Petro kuondoka, Mdo 10:19, 20.
-  Alitabiri kwa midomo ya Agabo, Mdo 21:10, 11.
-  Anasema na watakatifu wenye masikio, Ufu 2:7.
5.      Roho Mtakatifu anaomba
-  Mwenyewe ni Roho wa neema na kuomba, Zek 12:10.
-  Anawaombea watakatifu kwa kuugua kusikoweza kutamkwa, Rum 8:26.
-  Ametumwa kulia “ABBA” ndani ya wana wa Mungu, Gal 4:6.
6.      Roho Mtakatifu anaongoza
-  Alimwonya na kumwongoza Simeoni, Lk 2:25, 26.
-  Aliwaongoza watumishi wa Mungu, Mdo 13:4.
-  Aliwakataza na kuwapa maono akina Paulo na Timotheo, Mdo 16:6-10.
7.      Roho Mtakatifu anachunguza na kushuhudia
-  Anachunguza mafumbo ya Mungu, 1Kor 2:10-13.
-  Mwanadamu hawezi kujiepusha naye, Zab 139:7.
-  Atushuhudia wokovu.
B: TABIA YAKE ROHO MTAKATIFU
Roho Mtakatifu anatajwa kwa majina mbalilmbali katika Biblia ambayo maana yao yanafunua tabia yake wazi.
1.      Ndiye Roho wa Mungu
-  Alikuwapo wakati dunia inaumbwa, Mwa 1:2.
-  Alikuwapo wakati wa kutolewa maandiko, 2 Pet 1:20, 21.
-  Alikuwapo wakati wa kutungwa mimba kwa Mariamu, Mt 1:18.
2.      Ndiye Roho wa kweli
-  Anasimama kwenye kweli yote, Yn 14:17.
-  Anapinga na kudhihirisha uongo wote, Mdo 5:1-3.
-  Watakatifu wanamtambua na kujazwa tabia naye, Yn 14:17.
3.      Ndiye Roho Mtakatifu
-  Mwenyewe ni mtakatifu na anawatakasa wale ambao wanamtii Mungu, 1Thes 4:7, 8; 1 Pet 1:2.
4.      Ndiye Roho ufunuo
-  Anajua yote kabisa, mtu hawezi kujiepusha naye, Zab 139:7.
-  Anachunguza yote, hata mafumbo ya Mungu, 1 Kor 2:10.
-  Anataka kuwapa watakatifu hekima ya ufunuo katika kumjua pamoja na yote waliyopewa ndani ya Kristo, Efe 1:17, 18.
-  Anafunua yatakayotokea mbeleni, Ufu 1:9-11; Yoe 2:28.
5.      Ndiye Roho wa upendo
-  Tabia yake ni upendo, na anataka kuwajaza wakristo upendo wake, 2 Tim 1:7.
6.      Ndiye Roho wa hekima, shauri, uweza, maarifa na kumcha Bwana
-  Roho huyo alikaa juu yake Yesu, Isa 11:1-2.
7.      Ndiye Roho wa utukufu
-  Anawakalia wale wanaolaumiwa kwa ajili ya jina lake Yesu, 1 Pet 4:14; Mdo 6:10, 15.
-  Akipata kutawala katika maisha ya mkristo, inatokea kuwa mkristo huyo anabadilishwa na kufanana na Bwana toka utukufu hata utukufu, 2 Kor 3:18.
            C: ROHO MTAKATIFU KWA MIFANO YAKE
Mifano inatumiwa ili kusaidia kuelewa mambo zaidi. Kwa kuwa Roho Mtakatifu hana  umbo la binadamu, anaoneshwa katika Biblia kwa mifano mbalimbali kusudi tumwelewe jinsi alivyo.
1.      Roho Mtakatifu alijifunua akishuka kama HUA
-  HUA ni ndege mzuri , anapendeza na ni mpole, Mt 3:16.
-  Roho Mtakatifu aliposhuka kama HUA anaonesha uzuri, mapenzi, wema na usafi, Zab 143:10.
2.      Roho Mtakatifu alitokea kama MOTO
-  Moto huangaza na kufunua, hupima na kuyeyusha, hubagua na kupambanua, husafisha, kubadilisha na huunganisha, ndivyo alivyo Roho Mtakatifu katika uweza wake, Mdo 2:3, 4.
3.      Roho  Mtakatifu anafanana na UPEPO
-  Upepo huvuma upendako bila kuonekana wala kuzuiwa na mtu, sawasawa na Roho Mtakatifu katika kazi zake. Haongozwi na mtu kwa sheria yake, anatenda mwenyewe kama apendavyo, Mdo 2: 2-4; Yn 3:8, 9.
4.      Roho Mtakatifu anatokea kama CHEMCHEMI ya maji
-  Maji yana nguvu ya kuondoa kiu kwa mtu, kadhalika Roho Mtakatifu ana uwezo wa kuondoa kiu ya kufanya maovu kwa mtu, Yn 7:37-39.
5.      Roho Mtakatifu ni kama MAFUTA
-  Mafuta hurainisha, hurahisisha, hudumisha, huponyesha na huwezesha, Mdo 10:38.
-  Mafuta ni mfano wa uzima wa milele katika Roho wa Mungu, Mt 25:3-8.
-  Mafuta ni mfano wa shangwe katika haki, Ebr 1:9,1 0.
-  Mafuta ni mfano wa umoja na upendo ambao unaonekana kati yao waongozwao na Roho Mtakatifu, Zab 133: 1, 2.
6.      Roho Mtakatifu ameitwa MUHURI
-  Muhuri huthibitisha na hudhihirisha haki au uhalali wa kitu au mtu, 2 Tim 2:19.
7.      Roho Mtakatifu anapokewa kama ARABUNI
-  Watakatifu wamepewa kama arabuni mioyoni mwao, wana hakika juu ya urithi wao, 2Kor 1:21, 22; Efe 1:14, 15.
D: HABARI ZAIDI JUU YA KAZI ZAKE ROHO MTAKATIFU
Roho Mtakatifu anafanya kazi muhimu sana katika ulimwengu, katika maisha ya mkristo na katika kanisa kwa ujumla.
1.      Roho Mtakatifu anauhakikishia ulimwengu
-  Kwa habari ya dhambi, Yn 16: 9.
-  Kwa habari ya haki, Yn 16:10.
-  Kwa habari ya hukumu, Yn 16:11.
2.      Roho Mtakatifu anamshirikisha mtu uzima wa milele
-  Roho Mtakatifu anaumba uzima wa milele ndani ya roho ya mtu aliyezaliwa mara ya pili, Yn 3:5; Efe 2:5.
-  Wanaomwani Yesu  wanaishi na kuenenda kwa Roho wa Mungu, Gal 5:25.
3.      Roho Mtakatifu anamwacha mwanadamu huru na sheria ya dhambi na mauti
-  Kwa maana sheria ya Roho wa uzima inamwacha huru mbali na sheria ya dhambi, Rum 8:2-4.
-  Tena hakuna hukumu ya adhabu juu yao walio katika Kristo, wamekwisha kuhuishwa rohoni, tena watahuishwa kwa mwili pia watakapofufuka kwa nguvu ya Roho, Rum 8:1, 8-11.
4.      Roho Mtakatifu anamshuhudia anayemwamini Yesu kuwa ni mtoto wa Mungu
-  Roho Mtakatifu hushuhudia na roho zetu kuwa tu wana wa Mungu, Rum 8:16.
-  Roho Mtakatifu anamshuhudia mkristo udugu naye  Kristo mwana wa Mungu, Gal 4:6.
5.      Roho Mtakatifu anawapa wakristo nguvu
-  Anawapa watu wa Mungu nguvu kwa utu wa ndani, Efe 3:16, 17.
-  Anawapa nguvu ya kuwa mashahidi wake Kristo, Mdo 1:8, 9.
-  Anawapa nguvu ya kuwa waaminifu hata kufa, Mdo 7: 54-58.
6.      Roho Mtakatifu anawakumbusha walioamini yote aliyosema Yesu
-  Atawakumbusha yote, Yn 16:13-15.
7.      Roho Mtakatifu anawajaza walioamini shukrani na shangwe
-  Roho Mtakatifu anawapa wakristo nyimbo na tenzi nzuri, Efe 5:18-20.
-  Anawawezesha kuimba na kusema kwa moyo wote, Zab 86:12, 13.
-  Anawajaza furaha hata wakifungwa na kuteswa, Mdo 16:25-33.
8.      Roho Mtakatifu ni msaidizi wa walioamini
-  Anawasaidia kuyajua waliyokirimiwa na Mungu katika Kristo, 1Kor 2:12.
-  Anawasaidia katika mambo ya kiroho, 1Kor 2:13
-  Anawasaidia katika udhaifu, Rum 8:26.
-  Anawakumbusha yote aliyosema Yesu, Yn 14:26.
9.      Roho Mtakatifu anamtukuza Yesu mwana wa Mungu
-  Anawaongoza katika kweli yote na kumtukuza Yesu, Yn 16:13, 14.
E: UBATIZO KATIKA ROHO MTAKATIFU
1.      Mungu ametoa ahadi juu ya ubatizo katika Roho Mtakatifu
-  Ahadi hii ilinenwa zamani zile za nabii Yoel, Yoel 2:28-32.
-  Yesu mwenyewe aliwaahidi wanafunzi wake, Yn 16:7; Mdo 1:8.
2.      Mambo yaliyokuwa ya lazima kutimia kabla ya ubatizo katika Roho Mtakatifu kutokea ulimwenguni
-  Ilimbidi Yesu Kristo kuja ulimwenguni kwanza, Gal 4:4-6.
-  Ilimbidi Yesu kufa msalabani kusudi upatanisho kati ya wanadamu na Mungu upatikane, 1Tim 2:5, 6; Ufu 5:9, 10.
-  Ilimbidi Yesu kufufuka na kuondoka duniani akapandishwa mbinguni, Mdo 2:32, 33; Yn 16:7.
3.      Maana yake “Kubatizwa katika Roho Mtakatifu”
Neno hili ‘ubatizo’ linatoka katika lugha ya kiyunani yaani ‘BAPTISMA’ maana yake ni “kuzama au kuzamisha”. Kwa hiyo kubatizwa katika Roho Mtakatifu ni harakati za utendaji kazi wa Roho Mtakatifu juu na au ndani ya muumini ambapo anakuwa amejazwa uwezo na nguvu maalumu.
-  Kuna tofauti kati ya kuzaliwa kwa Roho mara ya pili na kubatizwa katika Roho Yule mmoja.  
Yaani ni hivi:
                  Katika kuzaliwa kwa Roho mara ya pili ni kwamba mtu anaumbwa upya kwa uzima wa milele, 
                 Yn 3:5-8, ambapo kubatizwa  katika Roho ni kujazwa uwezo na nguvu maalumu, Lk 3:16, 17.
-  Kubatizwa katika Roho Mtakatifu ni kupokea nguvu ya ajabu na kuwa mashahidi wa Yesu Kristo duniani, Mdo 1:8.
-  Kubatizwa katika Roho Mtakatifu kunaleta ujasiri wa kumshuhudia Yesu kuwa Bwana na Mwokozi, Mdo 4:8
-  Kubatizwa katika Roho Mtakatifu kunaleta karama, 1Kor 12:4-12, Mdo 10:46.
-  Mtu akijazwa Roho Mtakatifu anajazwa an upendo wa Mungu, Rum 5:5, 6.
4.      Habari ya kuupokea ubatizo katika Roho Mtakatifu
-  Waliozaliwa mara ya pili, wenye moyo safi, wanaomtii Mungu ndio wanaweza kuupokea ubatizo katika Roho Mtakatifu, Yn 14:17; Mdo 5:32; 8:18-21; 15:7-11.
-  Ahadi hii ni kwa ajili ya wakristo wote wa siku za mwisho, Mdo 2:39.
5.      Kufanywa upya na kuenenda katika Roho Mtakatifu na nguvu zake
-  Ubatizo katika Roho Mtakatifu unafungua mlango wa mkristo kujaa nguvu na uweza kila wakati akiishi nuruni maishani mwake, Yn 7:38; Mdo 6:5.
-  Kubatizwa katika Roho Mtakatifu ni mwanzo wa kuenenda katika ushindi, 2Kor 4:16, 3:18.
-  Kubatizwa katika Roho Mtakatifu unapokewa mara moja tu katika maisha ya mtu, Zab 51:10-12; Rum 11:29.
F: KARAMA ZA ROHO MTAKATIFU
Nyakati zilizopita Roho Mtakatifu alijidhihirisha duniani kwa namna mbalimbali, lakini kwa wakati huu wa mwisho anajidhihirisha hasa kwa karama zake katika kanisa. Matokeo haya yana maana sana katika kazi ya kuieneza injili na kuyatimiza mapenzi ya Bwana.
1.      Tupambanue KARAMA ZA ROHO na karama zingine zitokazo kwa Mungu
-  Wokovu na uzima wa milele ni karama za Mungu walakini haina maana sawa na karama za Roho Mtakatifu, Rum 6:23.
-  Kula na kunywa ni karama ya Mungu walakini maana yake si sawa na karama za Roho Mtakatifu, Mhu 3:13.
Roho Mtakatifu mwenyewe pamoja na matokeo yake yote yameitwa KIPAWA kwa jumla, walakini maneno haya matatu KARAMA ZA ROHO yanahusu kitu cha pekee ndani yake, Mdo 2:38.
-  KARAMA ZA ROHO ni karama ambazo mkristo anapokea akiwa anabatizwa ubatizo wa Roho Mtakatifu tu. Ni karama za uwezo wa pekee,tena haziwezi kuwepo kwa njia zingine, 1Kor 12:4.
-  Mkristo anaweza kutumika kweli katika karama hizo kwa njia ya ufunuo wa roho tu, 1Kor 12:7, 8.
2.      Pana tofauti za KARAMA ZA ROHO
-  KARAMA ZA ROHO zinahesabiwa na kutajwa kuwa ziko tisa (9) kwa idadi yake, 1Kor 12:4-9.
I.                    Neno la hekima
II.                  Neno la maarifa
III.                Imani
IV.                Karama za kuponya
V.                  Matendo ya miujiza
VI.                Unabii
VII.              Kupambanua roho
VIII.            Aina za lugha
IX.                Tafsiri za lugha
I.                    KARAMA YA NENO LA HEKIMA
-  Ni elimu kutokana na ufunuo wa roho, hutumiwa wakati wa mahitaji yake, Mdo 6:9, 10, 1Kor 2:6, 7.
-  Karama hii inawasaidia viongozi waliowekwa na Mungu kuliongoza kanisa lake, Mdo 6:2, 3.
-  Kwa karama hii, Roho alishirikiana na mitume katika kukata shauri, Mdo 15:28.
II.                  KARAMA  YA NENO LA MAARIFA
-  Karama hii inawawezesha walioitwa na Mungu kufundisha neno lake, 2Tim 2:15.
-  Inawawezesha kuelewa uhusiano uliopo kati ya agano la kale na agano jipya, Mdo 2:15, 16.
III.                KARAMA YA IMANI
-  Sivyo kuwa na imani ya kuupokea wokovu bali hii ni imani maalum inayoletwa na Roho, kusudi jina la Yesu litukuzwe kwa ishara zinazofuata tendo la imani hiyo. Matokeo yake yanajenga kanisa katika kumtegemea Yesu zaidi, Mk 16:18; 1Kor 13:2.
IV.                KARAMA ZA KUPONYA
-  Karama za kuponya siyo elimu ya uganga kwa kusoma shuleni, bali ni matokeo na uwezo katika Roho Mtakatifu, Mdo 3:4-9.
V.                  KARAMA YA MATENDO YA MIUJIZA
-  Kutoa pepo wachafu, Mdo 8:6, 7.
-  Wafu kufufuliwa, Mdo 9:40.
-  Kulipiza kisasi, Mdo 13:9-11.
VI.                KARAMA YA UNABII
                                                  Neno hili limetafsiriwa kuwa ni KUHUTUBU kwa Kiswahili, maana yake ni KUTABIRI 
                         au KUSEMA KWA UNABII, yaani si kuhutubu kwa njia ya kujitayarisha mwenyewe au 
                         kwa kusudi la mtu, bali ni kwa kujaliwa na Roho, 1Kor 14:1. 
 - Unabii wa karama za roho unaweza kutokea:-
i.                    kwa kufunua wazi mambo yaliyokwisha kufanyika katika siri, Mdo 5:1-5.
ii.                  tena kwa kuyafunua yatakayotukia mbeleni, Mdo 11:27, 28.
-  Unabii wenyewe unatolewa kwa njia mbili, yaani:-
i.                    mara moja, neno kwa neno jinsi mtu anavyojaliwa na Roho Mtakatifu, Mdo 21:11-14.
ii.                  tena unabii unatolewa rohoni mwa mtu, lakini hujulishwa wengine kwa maneno anayoyachagua mwenyewe, Mdo 20:29-31.
-  Unabii wa Roho Mtakatifu unaleta maneno ya kujenga, kufariji, kutia moyo na hata ukiwa wa kuonya na kuongoza roho yake ni ya upendo wa Yesu, 1Kor 14:3.

VII.              KARAMA YA KUPAMBANUA ROHO
-  Karama hii ni uwezo maalumu wa Roho Mtakatifu kupambanua roho ndani ya matokeo na maneno mbalimbali katika watu, Ufu 2:2.
-  Katika kupambanua hivi kuna matokeo ya roho tatu, Mdo 16:16-18, 1Yoh 4:1.
i.                    Roho wa Mungu
ii.                  roho ya mwanadamu
iii.                roho chafu
VIII.            KARAMA YA AINA ZA LUGHA
-  Karama hii hufunuliwa katika uwezo wa kusema kwa lugha ngeni bila kujifunza, lugha hizo zinaweza kuwa za wanadamu au za malaika, Mdo 2:4, 11; 1Kor 13:1; 14:2.

IX.                KARAMA YA TAFSIRI YA LUGHA
-  Karama hii siyo maarifa ya kujipatia kwa kujifunza bali ni uweza unaotokea mtu akipewa na roho.
-  Mwenye karama hii anaweza kujaliwa kutafsiri, mwingine akinena kwa lugha, 1Kor 14:27.
-  Mtu mwenye karama hii anaweza kujitafsiri mwenyewe, kusudi wenzake wajengwe akijaliwa na Roho, 1Kor 14:13.